Monday, September 30, 2013

SERIKALI YAFUNGIA MWANANCHI & MTANZANIA

Dar es Salaam. Serikali jana ilitangaza kuyafungia magazeti ya Mwananchi na Mtanzania kuanzia Septemba 27, 2013 kwa kile ilichoeleza kuwa ni mwenendo wa magazeti hayo kuandika habari za uchochezi na uhasama. Taarifa iliyotolewa jana na Mkurugenzi wa Habari (MAELEZO), Assah Mwambene ilisema gazeti la Mwananchi limefungiwa kwa siku 14 na gazeti la Mtanzania limefungiwa kwa siku 90. Magazeti hayo yamefungiwa kutokana na kuandika habari na makala zilizoelezwa zina nia ya kusababisha wananchi wakose imani kwa vyombo vya dola na kuhatarisha amani. “Gazeti la MWANANCHI limefungiwa kutochapishwa kwa siku kumi na nne(14) kuanzia 27 Septemba, 2013. Adhabu hii imetangazwa kwa Tangazo la Serikali(Government Notice )Namba 333 la tarehe 27 septemba,2013,” yasema taarifa hiyo. Kwa taarifa zaidi, tazama nakala ya tamko kamili la serikali juu ya kufungiwa kwa magazeti ya Mwananchi na Mtanzania hapo chini. TAMKO KAMILI LA SERIKALI Serikali imeyafungia kutochapishwa Magazeti ya MWANANCHI na MTANZANIA kuanzia 27 Septemba, 2013 kutokana na mwenendo wa magazeti hayo kuandika habari na makala za uchochezi na uhasama kwa nia ya kusababisha wananchi wakose imani kwa vyombo vya dola hivyo kuhatarisha amani na mshikamano ulipo nchini. Gazeti la MWANANCHI limefungiwa kutochapishwa kwa siku kumi na nne(14) kuanzia 27 Septemba, 2013.Adhabu hii imetangazwa kwa Tangazo la Serikali(Government Notice )Namba 333 la tarehe 27 Septemba, 2013. Gazeti la MWANANCHI limepewa adhabu hiyo kutokana na hivi karibuni kuchapisha habari zenye mwelekeo wa uchochezi na uvunjifu wa amani,mfano tarehe 17 Julai, 2013 katika toleo Namba 4774 ilichapisha habari isemayo “MISHAHARA MIPYA SERIKALINI 2013” kwa kuchapisha waraka uliozuiliwa kwa matumizi ya vyombo vya habari waraka huo ulikuwa wa Siri haukupaswa kuchapishwa Magazetini. Aidha, katika toleo la Jumamosi, tarehe 17 Agosti, 2013 lilichapisha habari yenye kichwa kisemacho “WAISLAM WASALI CHINI YA ULINZI MKALI” habari hiyo ilikolezwa na picha ya mbwa mkali mwenye hasira.Habari na picha hiyo ilitoa tafsiri ya kuwa Jeshi la Polisi lilipeleka Mbwa katika maeneo ya ibada ya waumini wa dini ya kiislam.Jambo ambalo halikuwa la ukweli. Jeshi la Polisi katika doria siku hiyo halikupeleka mbwa katika maeneo ya Misikiti.Serikali na jeshi la Polisi linaheshimu na kuzingatia maadili ya dini ya Kiislamu na kwa hiyo Jeshi lake haliwezi kupitisha au kuingiza mbwa katika maeneo ya ibada. Hivyo basi,kwa gazeti hili kuchapisha habari iliyokolezwa na picha ya mbwa ni uchochezi wa kulichonganisha Jeshi la Polisi na waumini wa dini ya kiislam mbwa ni najisi hapaswi kuingia katika maeneo ya ibada.